Na Peter Mkwavila,Dodoma.
WATANZANIA wameshauriwa kusaidia vituo vya kulelea watoto yatima na wale wenye mahitaji maalumu ili kupunguza mzigo wa gharama mbalimbali zikiwemo za kielimu,kiafya na chakula.
Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa kituo cha kulelea Watoto Yatima cha Nyumba ya Matumaini,Sista Aurea Kyara wakati akipokea msaada wa vyakula na vifaa mbalimbali vya usafi kutoka Jumuiya ya Mtakatifu Simon Zelothe ya Area D mjini hapa.
Kyara alisema kituo hicho kinakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo grarama za kumudu kuwasomesha watoto pamoja na matibabu na chakula.
“Ikiwa Watanzania watajenga tabia ya utamaduni wa kuwasaidia watoto wanaoachwa na wazazi wao, itasaidia kupunguza idadi kubwa ya watoto yatima kwenye vituo vya kulelea watoto hawa,”alisema.
Alisema kituo hicho kinapokea watoto kuanzia miaka miwili na nusu na kuendelea kutoka Idara ya Ustawi wa Jamii ambao waliondokewa za wazazi na wengine kukosa msaada toka kwenye familia husika.
Hata hivyo, alisema watoto hao wakifika darasa la saba hurudishwa nyumbani kwa ndugu zao ili waweze kuendelea kulelewa huko.
“Changamoto nyingine tunayoipata ni watoto tunaowaopeleka mara baada ya kumaliza darasa la saba wanarudi kwa kushindwa maisha na wengine kutakiwa kuolewa hata kama wamefaulu kuendelea na masomo,”alisema.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mtakatifu Simon Zelothe, Joseph Mariti, alisema wanajumuiya hiyo waliamua kuchanga ili kukisaidia kituo hicho kiweze kushiriki kwa pamoja katika kusherekea sikukuu ya Pasaka kama watoto wengine.
“Sisi kama Jumuiya ya kikristo tumeamua kuchanga misaada hii ili watoto hawa waweze kusherekea sikukuu ya pasaka sawa na watoto wetu,”alisema Mariti.
Alisema hatua hiyo pia ni miongoni mwa matendo wanayojifunza wakristo wakati huu wa Kwaresima ya kujitolea na kuwasaidia wengine ambao wanatakiwa kuyaishi katika maisha ya kila siku.
Mhariri:denice kazenzele
march 21/2016
No comments
Post a Comment