Leo ni siku ambayo ilikuwa 
ikisubiriwa sana na mashabiki wengi wa soka la Tanzania, leo ndio siku 
ambayo unapigwa mtanange wa Dar es Salaam Darby (Yanga vs Simba) mechi 
hii inatajwa kuwa miongoni mwa Derby kubwa barani Afrika lakini ikiwa ni
 Derby yenye upinzani mkubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Simba na Yanga zinakutana leo 
kwenye raundi ya nne ya VPL lakini ikiwa ni mechi ya kwanza 
inayozikutanisha timu hizo msimu huu, hapa chini nimekuwekea vitu muhimu
 unavyotakiwa kuvijua kabla ya mechi haijapigwa ili wakati wa mchezo 
utapofika unakuwa unajua vizuri nini kinaendelea.
Matokeo ya timu zote msimu huu mpaka sasa 
Baada ya mechi tatu kuwa 
zimechezwa hadi sasa, timu zote zimeshinda michezo yote mitatu Simba 
imeshinda mechi zake dhidi ya African Sports na Mgambo JKT ugenini 
kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga mechi yao ya tatu walishinda wakiwa 
kwenye uwanja wa taifa dhidi ya Kagera Sugar. Yanga mechi zao zote 
wameshinda wakiwa kwenye uwanja wa taifa dhidi ya Coatal Union, Tanzania
 Prisons na JKT Ruvu.
Vita ya Hamisi Kiiza vs Amis Tambwe
Hawa ni washambuliaji wawili 
ambao leo watakuwa wakicheza dhidi ya vilabu vyao vya zamani. Kiiza 
alikuwa Yanga kwasasa yupo Simba wakati Tambwe alikuwa Simba na sasa 
yupo Yanga na wote kwa pamoja wamekuwa na moto wa ajabu katika kutupia 
kambani msimu huu.
Kiiza
Mpaka sasa anaongoza kwa kutupia 
nyavuni akiwa amefunga bao tano baada ya kufunga kwenye mechi ya kwanza 
bao moja, mechi ya pili bao moja na mechi ya tatu bao tatu na hii ikiwa 
ni hat-trick ya kwanza kwa msimu huu lakini ikiwa ni hat-trick yake ya 
kwanza pia akiwa Msimbazi.
Tambwe
Amefunga jumla ya bao tatu hadi 
sasa. Alifunga bao moja kwenye mechi ya kwanza, halafu mechi ya tatu 
akatupia mbili dhidi ya JKT Ruvu wakati Yanga ilipoibuka na ushindi wa 
goli 4-1.
Mtiririko wa matokeo
Yanga
Walianza kwa ushindi wa goli 2-0 
dhidi ya Coasta Union, wakapata ushindi wa goli 3-0 dhidi ya Tanzania 
Prisons na mechi ya tatu wakashinda kwa goli 4-1 dhidi ya JKT Ruvu. Leo 
wanakutana na ‘mnyama’ hii ina maana kama wanaendelea kwa mfululizo huo 
wataibuka na goli tano.
Simba
Walianza kwa ushindi wa goli 1-0 
dhidi ya African Sports kwenye mechi ya kwanza, mechi ya pili wakashinda
 kwa goli 2-0 dhidi ya Mgambo JKT na mechi ya tatu wakaibuka na ushindi 
wa goli 3-1 dhidi ya Kagera Sugar. Kama wataendelea na mfululizo huohuo 
inamaana leo watafunga bao nne.
Magoli ya kufungwa
Kila timu imeruhusu goli moja 
kwenye mchezo wake wa tatu, timu zote zimefungwa kwenye uwanja wa taifa 
ambao zinautumia kama uwanja wao wa nyumbani na kila timu imefungwa 
kwenye mchezo iliopata ushindi mkubwa.
Yanga
 Imefungwa goli moja wakati 
ilioibuka na ushindi wa goli 4-1 dhidi ya JKT Ruvu mchezo uliochezwa 
kwenye uwanja wa taifa. Yanga wamefunga magoli tisa kwenye mechi tatu 
walizocheza.
Simba
Ilifungwa goli moja kwenye 
ushindi wake mkubwa msimu huu hadi sasa ilipoifunga Kagera Sugar kwa 
goli 3-1 kwenye uwanja wa taifa wakati wao wakiwa wamefunga jumla ya 
magoli sita hadi sasa.
Historia ya timu hizo kwenye mchezo wa Dar es Salaam Derby
Timu hizi tayari zimekutana mara 
79 kwenye mechi za ligi kuu Tanzania bara, mchezo wa leo utakuwa ni wa 
80 huku ukiwa ni wa kwanza kwenye msimu huu wa 2015/16.
Takwimu zinazungumaje?
Mabinwa watetezi wa ligi hiyo 
timu ya Yanga wanaongoza kwa kuwafunga watani zao Simba wakiwa 
wameshinda mechi 29 kati ya 79 wakati Simba wao wameifunga Yanga kwenye 
mechi 23 kati ya 79 huku mechi 27 kati ya 79 zikiwa nisare.
Matokeo ya msimu uliopita
Kwenye mechi ya kwanza msimu 
uliopita timu hizo zilitoka sare lakini mechi ya pili (marudiano) Simba 
iliitandika Yanga kwa bao 1-0 lililofungwa na mshambuliaji wa Uganda 
Emanuel Okwi.
Maswali mawili ya kujiuliza kabla ya mchezo wa leo
1. Je, Yanga ambao ni mabingwa 
watetezi wa ligi kuu Tanzania bara watalipa kisasi cha kufungwa mara kwa
 mara siku za hivi karibuni au Simba wataendelea kupeleka kilio 
Jangwani?
2. Je, ni nani kati ya Kiiza na Tambwe atakaepeleka kilio kwenye timu yake ya zamani?

No comments
Post a Comment