MGOMBEA wa urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk John Magufuli, amewataka wakazi wa Biharamulo mkoa wa Kagera, kumwachia mgogoro wa wafugaji na wakulima kwa kuwahakikishia kwamba akichaguliwa, ataushughulikia.
Alitoa ahadi hiyo jana mjini Biharamulo, alikohutubia umati wa wananchi, baada ya kuhitimisha ziara za kampeni mkoani Kigoma.
Alisema anafahamu mgogoro uliopo kati ya makundi hayo.
“Hilo mniachie nitalishughulikia. Nina hakika mbunge mtakayemchagua, atashirikiana na mimi kutatua mgogoro huo,” alisema Dk Magufuli.
Magufuli aliteka maeneo mengi mkoani Kigoma na sehemu za wilaya za Biharamulo (Kagera) na Chato (Geita) kutokana na wingi wa watu waliojitokeza kwenye mikutano ya hadhara pamoja na waliomsimamisha njiani.
Akiwa njiani kutoka Biharamulo kwenda Chato, ambako ni nyumbani kwake, ilimchukua muda mrefu njiani kutokana na kusimamishwa sanjari na kushangiliwa na umati wa watu katika vijiji mbalimbali na kumfanya asimame kuwasalimia.
Miongoni mwa vijiji ambavyo mgombea huyo alilazimika kusimama ni pamoja na Igalula, Mwangaza na Kachwamba, ambako alikuwa akimnadi na kumwombea kura mgombea ubunge wa CCM, Medard Kalemani.
Aidha, Magufuli aliahidi atakapokuwa rais, atahakikisha barabara inayounganisha Biharamulo na Chato, inakarabatiwa. Dk Magufuli alikwenda Chato jana kabla ya kuendelea na ziara za kampeni kwenye mikoa ya Geita na Kagera iliyoko Kanda ya Ziwa.
Amlilia mwalimu wake Baada ya kuhitimisha kampeni katika Wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma, Magufuli alikwenda moja kwa moja Biharamulo, ambako pamoja na kuhutubia maelfu ya watu, pia alikwenda kuhani msiba wa mwalimu wake wa shule ya msingi, Cornel Pastory nyumbani kwake wilayani humo.
Akizungumza kwenye mkutano wa kampeni baada ya kutoka nyumbani kwa mwalimu wake, ambako alishiriki kuweka shada kwenye kaburi lake, alisema historia yake imetokana na Biharamulo.
CREDITY: HABARI LEO
No comments
Post a Comment