Na Peter Mkwavila,Kongwa.
WANANCHI wa Kijiji cha Matongoro wilayani Kongwa mkoani hapa wamemtuhumu mwenyekiti wa kijiji hicho Moses Daudi kwa kile walichodai kuuza chakula cha msaada kilichopelekwa kwa ajili ya vikongwe na walemavu.
Wakizungumza na Nipashe jana kijijini hapo wananchi hao walidai kuwa walipata taarifa ya kuwepo kwa chakula cha msaada magunia 59 ambazo zilikuwa kwa ajili ya kugawiwa vikongwe na walemavu .
Moja wa wakazi wa kijijiji hicho Mathayo John alisema kuwa kungundulika kwa wizi huo ni baada ya baadhi ya wakazi wenzao kukutwa wakiwa na magunia ya mahindi hayo na walipotaka kufahamu wamepata wapi walieleza kuwa wameuziwa na mwenyekiti huyo wa kijiji.
Naye Ndonye Chedego alisema kuwa kutokana na tabia hiyo ameiomba serikali kuhakikisha kumchukulia hatua za kisheria mwenyekiti huyo na wengine watakaobainika kujihusisha na wizi huo wa chakula cha msaada kilichotolewa kwa ajili ya jamii hiyo isiyojiweza.
“Kitendo hicho ni cha kifisadi na kinatakiwa kulaniwa kutokana na kufanywa na viongozi wa serikali ya kijiji ambao wameingiwa na tamaa hivyo ni vyema wakachukuliwa hatua za kisheria”alisema Chedego.
Hata hivyo wananchi hao waliilalamikia pia kamati ya maafa ya kijiji hicho kutokana na kitendo chao cha kugawa chakula kwa watu ambao tayari walishapewa kwa awamu iliyopita.
“Utaratibu wa ugawaji wa chakula cha msaada hapa kijijini kwetu ulikiukwa lakini jambo la kushangaza ni baada ya kuwabaini watu wana magunia ya mahindi kitu ambacho kilitushtua sana,”alisema.Husseni Ally.
Naye mkazi mwingine Neeema Matande alisema kuwa wanashangazwa na kitendo cha utaratibu wa ugawaji wa chakula hicho kwani wanapewa watu wenye uwezo badala yawasio na uwezo.
“Hili ni jipu tunaiomba serikali kulitumbua jipu hili,ambalo limekiuka maadili ya uongozi,ukizingatia kitendo alichokifanya ameongeza machungu kwa vikonge na walemavu hao ambao wanatakiwa kusaidia kila siku.”alisema.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kijiji hicho,Moses Daud alipoulizwa na Nipashe kuhusiana na suala hilo la kutuhumiwa kuuza chakula cha msaada alikataa kuwa sio kweli bali mtendaji aliuza mahindi gunia nne tu kwa kushirikiana na kamati ya maafa ili kulipia nauli ya gari ambayo ilibeba mahindi hayo.
Imeandaliwa na Peter Mkwavila
Mhariri: Denice J Kazenzele
january 27/2016 {Jumatano}
No comments
Post a Comment