WAZIRI wa Nchi,Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene amewasimamisha kazi Wakurugenzi Watendaji wa Manispaa za Kigoma, mkoa wa Kigoma na Manispaa ya Mpanda Mkoa wa Katavi kwa tuhuma za kuridhia na kutekeleza maamuzi ambayo yameisasbabishia serikali hasara na upotevu wa fedha.
Akitoa taarifa hiyo jana kwenye mkutano wake na waandishi wa habari, Mkuu wa Kitengo cha mawasiliano Serikalini Ofisi ya Rais Tamisemi, Rebecca Kwandu, aliwataja wakurugenzi waliosimamishwa ni mhandisi Boniface Nyambele wa manispaa ya Kigoma anayekabiliwa na tuhuma za uuzaji wa nyumba za halmashauri bila kufuata sheria, kanuni na taratibu zilizopo bila kibali cha waziri mwenye dhamana kama sheria inavyoelekeza.
Pia alisema mkurugenzi wa manispaa ya Mpanda Suleiman Mkanga anakabiliwa na tuhuma za ununuzi hewa wa gari la kusomba taka kiasi cha Sh. milioni 92.75 na unadhilifu wa fedha za ujenzi wa skimu ya umwagiliaji ya Kakese kiasi cha Sh. milioni 294.
"Aidha Waziri ameagiza nafasi ya Mkurugenbzi wa Manispaa ya Kigoma ikaimiwe na mhandisi Sultan Ndilowa ambaye ni Mkuu wa Idara ya Maji, manispaa ya Kigoma na nafasi ya Mkurugenzi wa manispaa ya Mpanda ikaimiwe na Lauteri Kanoni ambaye ni katibu tawala msaidizi kutoka ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Katavi.
Pia Waziri Simbachawene aliwataka wakurugenzi watendaji wa mamlaka za serikali za mitaa kote nchini kuwa makini katika kutekeleza majukumu yao wafuate sheria, kanuni na taratibu zilizopo.
Alisema serikali haitasita kuchukua hatua za kinidhamu kwa watumishi wote ambao watakiuka matakwa ya sheria, kanuni na taratibu na kutoweka mbele maslahi ya umma.
mwisho
No comments
Post a Comment